Header Ads

SIENDI BUNGENI KUTAFUTA UTAJIRI, ANENA MGOMBEA WA CCM KALENGA


akisisitiza kazia atakazofanya

MGOMBEA ubunge wa uchaguzi mdogo jimbo la Kalenga kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Godfrey Mgimwa amesema ajaingia katika kinyang’anyiro hicho kwa lengo la kujitafutia utajiri.
“Wapo baadhi ya wanasiasa wanatafuta nafasi hii kwa lengo la kutafuta fedha na sio kuwatumikia wananchi; naomba mniamini mimi sijaingia kwa lengo hilo,” alisema.
Aliyasema hayo wakati wa kampeni zake alizofanya kwa nyakati tofauti jana katika vijiji vya Ilalasimba, Magubike, Kidamali na Nzihi vya kata ya Nzihi jimbo humo.
Mgimwa alisema ametoka kwenye ajira iliyokuwa ikilimpa vizuri kabla ya kuamua kutimiza ndoto yake ya siku nyingi ya kuwatumikia wananchi wa jimbo lake hilo.
“Kabla sijaja kugombea ubunge katika jimbo hili, nilikuwa mtumishi wa benki ya Stanibic makao makuu, huko nilikuwa nikilipwa vizuri sana, lakini nikasema siwezi kuendelea ili nirudi kwenu kwa lengo la kuwatumikieni,” alisema.
Aliwaomba wananchi wa kata hiyo na jimbo hilo kumuamini huku akisisitiza kwamba yeye ni msomi asiye na majivuno, msikuvu na asieyekata tama anapotaka jambo fulani lifanikiwe.
Katika mikutano kwenye kata hiyo, Mgimwa alisema atazibeba na kuzifanyia kazi nyingi ya ahadi ilizotolewa na marehemu baba yake, Dk William Mgimwa ili kuwaletea wananchi wa jimbo hilo maendeleo.
“Maendeleo ya jimbo hili yataletwa kwa kutekeleza Ilani ya CCM ya 2010 lakini kuna ahadi zilitolewa na marehemu Dk Mgimwa nje ya Ilani hiyo; niaminini nitazifanyia kazi,” alisema.
Akiwa katika kijiji cha Magubike alisema, wakati wa uhai wake Dk Mgimwa aliahidi kutoa mabati 400 kwa ajili ya ujenzi wa shule na zahanati ya kijiji hicho.
“Pamoja na ahadi hiyo aliahidi pia kutoa Sh Milioni moja kwa kikundi cha wajasiariamali wanawake, nazichukua ahadi hizo na nitazifanyia kazi,” alisema.
Akimuombea kura kwa wapiga kura wa kata hiyo, Naibu Katibu Mkuu wa CCM ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba alisema katika uchaguzi huo mdogo vyama vinavyoshiriki havishindanishi sera.
“Serikali ilikwishaundwa baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2010, kinachofanywa sasa ni kuziba nafasi ya mbunge aliyekuwepo, kwahiyo ahadi zinazotekelezwa ni zile zile zilizotolewa kupitia Ilani ya CCM na mgombea husika,” alisema.
Alisema hiyo ni sababu tosha kwa wana Kalenga kumpa kura za ushindi mgombea wa CCM kwa kuwa ndiye atakayemalizia utekeleza wa Ilani na ahadi za Dk Mgimwa kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Nchemba aliwahakikishia wana Kalenga kwamba Mgimwa ana kila sababu ya kumalizia kazi iliyoanza kutekelezwa na marehemu baba yake ili aweze kutengeneza jina.
“Mnajua Uchaguzi Mkuu uatakaoshindanisha sera za vyama mbalimbali utafanyika mwakani; kujiweke katika mazingira mazuri ni lazima Mgimwa atatekeleza ahadi anazowapeni katika uchaguzi huu mdogo,” alisema.

Uchaguzi mdogo wa jimbo la Kalenga unafanyika baada ya aliyekuwa mbunge wake, Dk Mgimwa kufariki dunia Januari 1, mwaka huu wakati akiendelea na matibabu yake nchi Afrika Kusini.
Powered by Blogger.