Header Ads

Auawa kwa kupigwa risasi

MKAZI wa Kijiji cha Masuguru, Kata ya Masagala, wilayani Kishapu, Juma Masalu (25), ameuawa kwa kupigwa risasi baada ya kuingia katika mgodi wa Almasi unaomilikiwa na Wiliamson Diamond.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Shinyanga, Kamishina Msaidizi Kihenya Kihenya, alisema tukio hilo lilitokea Juni 13, saa 5 usiku wakati Masalu na wenzake 20 walipoingia ndani ya mgodi huo kwa nia ya kuiba mchanga wenye madini ya almasi.
Kamanda Kihenya alisema wakati wakiiba mchanga huo, walinzi wa Kampuni ya Zenith wanaolinda mgodi huo waliwaona na kuanza kupambana nao kwa risasi huku wavamizi hao wakitumia mishale, mikuki na makombeo walivyoingia nazo mgodini.
Alisema Masalu alipigwa risasi sehemu za siri na kufariki wakati mwenzake Emmanuel Charles (23) mkazi wa Kata ya Majimaji mjini Maganzo alijeruhiwa kwa risasi mguu wa kushoto na anashikiliwa na polisi mkoani Shinyanga kwa mahojiano zaidi.
Hata hivyo, kamanda huyo alisema walinzi wawili wa kampuni hiyo ya ulinzi wametoroka na kutelekeza silaha zao kwa hofu ya kukamatwa baada ya kusababisha mauaji hayo.
Kihenya alisema Jeshi la Polisi linawatafuta wavamizi wengine 18 waliokimbia, ili wafikishwe mahakamani, na kutoa wito kwa vijana kujishughulisha na shughuli za uzalishaji mali badala ya kujiingiza katika uhalifu.
Powered by Blogger.