Header Ads

PINDA AIASA JUMUIYA YA UMOJA WA WAZAZI NCHINI Lazima iwe na kitu cha kujivunia

WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amesema Jumuiya ya Wazazi nchini ni miongoni mwa jumuiya inayoongoza na kusimamia masuala yote yanayohusu elimu, malezi bora kwa vijana wa taifa letu hivyo lazima iangalie jinsi ya kuweza kujipambanua katika utekelezaji wa Umoja wa Jumuiya yao.
 
Ametoa kauli hiyo leo mchana (Jumamosi, Februari 22, 2014), wakati akifungua rasmi semina ya siku tatu ya viongozi na watendaji wa Jumuiya ya Umoja wa Wazazi ngazi ya Taifa, Mikoa na Wilaya Tanzania inayofanyika kwenye Ukumbi wa NEC, Mkoani Dodoma.
 
Akizungumza katika ufunguzi huo, Waziri Mkuu Pinda  aliwaeleza wana jumuiya hao kuangalia malengo wanayojipangia aidha yawe ya muda mfupi au mrefu ili kuyatekeleza kwa kuzingatia yale mambo ya msingi na yenye kipao mbele kwa wananchi.
 
“Changamoto kubwa iliyopo mbele yenu kama viongozi na watendaji wakuu wa Jumuiya hii ni namna ya kutimiza malengo mliyojiwekea“.
 
Alisema, dhana ya Jumuiya ya Umoja wa Wazazi nchini ni kuongeza na kuboresha masuala yote yanayohusu Sekta ya elimu hapa nchini: ‘‘Tumieni semina hii kujipima kwamba mmefikia wapi katika utelelezaji wa malengo yenu kwa kuangalia mapungufu na maboresho katika jumuiya yenu‘‘. 
 
Jumuiya ya Wazazi ndio magwiji mnaoongoza kwa kuwa na shule nyingi hapa nchini, hivyo jumuiya yenu ijipange na kusimamia vema shule hizo ili kuwa vinara katika kuboresha masuala ya elimu hapa nchini. Akitoa mfano, alisema: “Kwanini shule za binafsi zinakuwa zinaongoza kuliko shule zilizopo ndani ya Jumuiya yenu, walau katika kumi bora iwepo shule moja kutoka Jumuiya ya Umoja wa Wazazi alisema Waziri Mkuu”. 
 
Kutokana na kauli hiyo, Waziri Mkuu aliiambia Jumuiya hiyo kutumia dhana ya elimu kama ngao yao katika kuleta maendeleo katika Sekta hiyo kwani Ilani ya chama cha Mapinduzi imetamka wazi kuongeza kasi ya upanuzi wa Elimu ya Awali, Msingi na Sekondari lengo ambalo ni moja ya jukumu kuu la msingi la Jumuiya ya Umoja wa Wazazi.
 
Aliendelea kusema kuwa Jumuiya ya Wazazi inajukumu la kusimamia masuala yote yanayohusu maadili, jukumu ambalo halina tofauti sana na jukumu la madhehebu ya dini kuzungumza bayana masuala ya malezi ya watoto na vijana ambayo yamekuwa yakiporomoka kila kukicha, hivyo Waziri Mkuu alisema, jumuiya hii itumia jukumu na nafasi waliyopewa kuhakikisha watoto wote walio ndani na nje ya jumuiya wanafundishwa maadili.
 
Waziri Mkuu aliendelea kusema kuwa, Jumuiya ya Umoja wa Wazazi ina majengo, viwanja na ardhi inayofaa kwa kilimo na shughuli za kiuchumi, tumieni fursa hizi kwa kujenga vyuo, kuanzisha miradi ya maendeleo ambayo itawasaidia katika kuongeza kipato katika jumuiya yenu.‘‘Mnachotakiwa ni kupanga bajeti zenu vizuri na kusimaia utekelezaji pamoja kusimamia vizuri miradi na fursa zinazojitokea“
 
Pamoja na hayo, Waziri Mkuu aliiomba Jumuiya ya Wazazi kujitokeza kuzungumzia masuala ya Dawa za Kulevya kwa kusema kuwa, wako vijana ambao wametumbukia katika dimbwi la Dawa za Kulevya ambaa pia wanahatarisha maisha yao kwa kupata UKIMWI: “Ni matumaini yangu kwamba Jumuiya ya Umoja wa Wazazi itakuwa mstari wa mbele kuelimisha jamii, kutoa ushauri kwa vijana kuhusu athari za dawa za kulevya, UKIMWI na  hata mkiweza kuanzisha vituo vya ushauri”, alisisitiza Waziri Mkuu.
 
“Ili kuweza kuwa na Jumuiya ya Wazazi imara ni dhahiri kuwa wanajumuiya wasimamie kanuni na maadili yanayoongoza jumuiya yao kwa kuwaasa kuacha kujiingaza katika makundi yasiyokuwa na msingi hasa kwa kutanguliza maslahi ya fedha katika kupata nafasi za uongozi katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu ambao huleta migawanyiko kati ya Viongozi na wanachama na wapiga kura”. Mzingatie masuala yanayohusu kujenga na kukuza utekelezaji wa jumuiya yenu ambayo itawasaidia kujenga jumuiya imara na kujenga chama imara kitakacho leta viongozi imara”alisisitiza Waziri Mkuu.
 
Mapema, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wazazi Taifa, Bw. Majura Bulembo, alisema lengo la semina hiyo ni kuwajengea uwezo na kuwaongeza ufanisi Jumuiya ya Wazazi katika utekelezaji  kazi zao na kuwasisitiza kuhudhuria semina hiyo ipasavyo ili kuweza kukumbusha mapungufu na changamoto zinazojitokeza katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu.
 
“Viongozi wamekuwa wakitumia vibaya nafasi za uongozi walizopewa kwa kujiona wao ndio viongozi wakuu kwa kujifanyia maamuzi yao, viongozi kama hao wataondolewa madarakani mara moja”.
 

 
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
S. L. P. 3021,
DAR ES SALAAM.
JUMAMOSI, FEBRUARI 22, 2014.
 
Powered by Blogger.