Header Ads

WAMILIKI WA VYUO NA SHULE BINAFSI WAINANGA SERIKALI IMESHINDWA KUBORESHA ELIMU

Mwenyekiti wa wamiliki kanda ya Nyasa, Chelestino Mofuga akitoa tamko

Mwakilishi wa Wizara ya Elimu Khadija Mchatta akitoa ufafanuzi, 

wamiliki wa taasisi binafsi za elimu kanda ya Nyasa wakisikiliza kwa makini
Add caption



Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Gerlad Guninita alipokuwa akitoa ufafanuzi wa mipango ya serikali katika kuboresha elimu
Katika picha ya pamoja
Katika picha ya pamoja
WAMILIKI wa shule na vyuo visivyo vya serikali, wameiponda Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi wakisema haina mipango dhabiti ya kuboresha elimu nchini.
Wamesema serikali imeshindwa kufanya maamuzi magumu ya kusimamia ufaulu wa alama 35 na badala yake inaruhusu wanafunzi wa kidato cha pili na cha nne wanaofeli kuendelea na masomo ya juu.
“Imekuwa kama maigizo ya wasanii kuhusu alama za ufaulu wa wanafunzi wa kidato cha pili na nne,” alisema Chelestino Mofuga ambaye ni Mwenyekiti wa shirikisho la mameneja na wamiliki wa shule na vyuo hivyo (TAMONGSCO) kanda ya Nyasa inayojumuisha mikoa ya Iringa,Njombe na Ruvuma.
Katika kikao chao cha siku mbili kilichofanyika mapema wiki hii mjini Iringa, Mofuga alisema kwa kidato cha pili TAMONGSCO ilishirikishwa na serikali na mapendekezo yao yalikuwa alama za ufaulu ziwe kati ya 35 na 40.
“Lakini baadaye serikali ilitangaza kuwa alama ya ufaulu itabaki kuwa 30 na kwamba nwanafunzi atakayeshindwa kufikia alama hizo atakariri darasa,” alisema.
Wakati wadau wa elimu wakishangilia uamuzi huo wa serikali, alisema Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kupitia barua yake ya Januari 16, mwaka huu, aliwataka wakuu wa shule zote nchini kuwaruhusu wanafunzi waliopata alama 20 na kuendelea waendelee na masomo ya kidato cha tatu, mwaka huu.
Mofuga alisema maamuzi hayo yanawafanya wanafunzi kutokuwa na ari ya kusoma wakiwa na imani kwamba wataruhusiwa kuendelea na masomo ya juu zaidi hata kama watafeli.
“Maamuzi hayo ya serikali yanachangia utovu wa nidhamu mashuleni, yanaandaa watazania wasioweza kufikiria vizuri, kupanga na kusimamia na kutathimini maendeleo ya nchi yao,” alisema.
Alisema maamuzi hayo katika ulimwengu huu wa utandawazi yanakaribisha ukoloni kwa mlango wa pili kwani itafika mahali wataalamu wengi wataagizwa kutoka nje.
Akiponda zaidi maamuzi ya wizara, Mofuga alisema yatawagawa watanzania na kusimika rasmi kundi la watu wachache wenye uwezo wa kupata elimu bora nje ya nchi kuendelea kuwa bora kuliko watoto wa wakulima.
Alisema katika ushindani wa soko la ajira ipo hatari kwa Tanzania kukosa ushindani na nchi za Afrika Mashariki na nyingine nyingi duniani kwa kukosa ubora wa elimu.
Akifungua mkutano huo, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Gerald Guninita alisema sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 1995 iko katika mchakato wa kufanyiwa marekebisho.
Alisema katika mchakato huo kuna mambo mengi sana yamerekebishwa ili kuendana na mahitaji ya utoaji wa elimu bora inayopatikana kwa wote na kwa usawa.
“Rasimu hii kwasasa inaangaliwa na wadau wengine na tuna imani itasainiwa na waziri muda si mrefu; ninawahakikishia kwamba sera hii itaondoa changamoto nyingi ambazo mnakabiliana nazo katika utoaji wa elimu bora,” alisema. 
Powered by Blogger.