Header Ads

KADA WA CHADEMA APINGA WANAOTAKA UDIWANI NA UBUNGE KUWA NA ELIMU INAYOANZIA KIDATO CHA NNE, ASEMA KIFUNGU HICHO KIKIFUTWA KITAWANUFAISHA BAADHI YA WABUNGE WA CCM

ABOU MAJEKI
Picha ya maktaba yetu ikimuonesha Jah People akijinadi kwa wapiga kura wa kata ya Makambako wakati wa mchakato wa kura za maoni za ubunge jimbo la Njombe Kaskazini kupitia CCM mwaka 2010; elimu yake ya msingi ilimfanya aeleweke vyema kwa wapiga kura wenye elimu kama yake na kumchagua kwa kura nyingi katika kura hizo za maoni
KADA maarufu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wa mjini Iringa, Abou Changawa amekiri kukoseshwa usingizi na pendekezo katika rasimu ya katiba Mpya linalotaka mgombea wa udiwani na ubunge angalau awe na elimu ya kidato cha nne.
Mbali na kuwa na elimu chini ya iliyopendekezwa katika rasimu hiyo, Changawa, maarufu kwa jina la Majeki ni mmoja kati ya wanasiasa wachache walioko kambi ya upinzani mjini Iringa wanaosifika kwa kujenga hoja.
“Naomba Mungu kila uchao, wabunge wa bunge hilo la Katiba wakikatae kifungu kinchotaka wagombea wenye elimu chini ya kidato cha nne wasigombee nafasi hizo za uwakilishi wa wananchi,” alisema.
Alisema kama kifungu hicho kitapita kitafutilia mbali ndoto zake za muda mrefu za kuwa diwani na baadaye Meya wa Manispaa ya Iringa.
“Katika siku zote za maisha yangu ya kisiasa nimekuwa nikisema, halmashauri ya manispaa ya Iringa inahitaji diwani mwenye uwezo wa hoja kama mimi ili awe meya,” alisema.
Aliwaomba viongozi na wabunge wa chama chake cha Chadema kukikataa kifungu hicho kwakuwa kitawanyima haki ya msingi ya kuchagua na kuchaguliwa watu wenye elimu kama yake.
“Tunataka Katiba Mpya lakini kipengele hicho kinataka kutopoteza kwenye siasa za uwakilishi tusio na elimu ya kidato cha nne,” alisema.
Majeki ambaye pia ni Mwenyekiti wa Klabu ya Soka ya Lipuli ya mjini Iringa aliwaomba watanzania kukikataa kufungu hicho kama kitapitishwa na bunge hilo maalumu la Katiba.
Kama kifungu hicho kitakataliwa imeelezwa na wadau wa siasa mkoani hapa kwamba kitaleta faraja kubwa kwa baadhi ya wabunge wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM) wenye elimu hiyo.
Mmoja wa wabunge hao ni Deo Sanga maarufu kwa jina la Jah People; mbunge huyu wa Njombe Kaskazini alichaguliwa kwa mara ya kwanza kushika wadhifa huo muhimu mwaka 2010.
Wakati wa kampeni zake za kutafuta ridhaa ya wana CCM kumchagua katika kura zake za maoni ili awe mbunge wao, Jah People alitumia wasifu wake wa elimu ya msingi kujinadi.
Katika moja ya mikutano ya kampeni zake iliyofanyika mwaka 2010 katika kata ya Makambako yalipo makazi yake, Jah People alijinadi kwamba yeye ni msomi mwenye ELIMU YA JUU YA DARASA LA SABA na ndio maana anamiliki mali nyingi ikiwa ni pamoja na kuwa Mkurugenzi Mkuu wa kampuni yake kubwa ya usafirishaji ya Jah People.
Elimu yake hiyo iliibua hoja katika uwanja wa siasa wa jimbo hilo kwa aliyekuwa Mgombea ubunge kupitia Chadema, Alatanga Nyagawa kuahidi kumfungulia mashitaka Jah People kwa madai kwamba alishindwa kumaliza elimu ya msingi ambayo kwa mujibu wa sheria ya nchi ni ya lazima.
“Kitaaluma mimi ni mwanasheria, na katika hili sina mzaha, nitampeleka Jah People Mahakamani kwasababu alikimbia elimu ya msingi ambayo ni ya lazima na kwa hilo amevunja sheria,” Nyagawa alisema mwaka 2010 wakati Chadema kikifanya uzinduzi wa kampeni za ubunge jimbo la Iringa Mjini katika uwanja wa Mwembetogwa.
Alisema kama ilivyo kwa nchi nyingi duniani ambapo elimu ya msingi imefanywa kuwa ya lazima, na wale wanaoikosa wametengenezewa utaratibu mwingine wa kuipata, atamfikisha mahakamani ili athibitishe kiwango chake cha elimu na hatimaye kulazimishwa kujiunga na Mpango wa Elimu ya Msingi kwa Walioikosa (Memkwa).
Hata hivyo Nyagawa hakutekeleza ahadi hiyo na mpaka sasa Jah People ni mbunge wa jimbo hilo ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Njombe.
Wasifu wa mbunge huyo uliopo katika mtandao wa bunge unaonesha kwamba alizaliwa Januari 1, 1965 na kuanza elimu yake ya msingi mwaka 1970 katika shule ya Ikwega iliyopo wilayani Mufindi mkoani Iringa; hata hivyo wasifu huo hauoneshi mwaka ambao mbunge huyo alimaliza elimu hiyo ya msingi.
Bila shaka kukataliwa kwa kifungu kinachotaka wagombea udiwani na ubunge wawe na elimu ya kidato cha nne kutakuwa na manufaa zaidi kwa mtu kama Jah People wa CCM zaidi ya manufaa ya Majeki ambaye hajui raha ya kuchaguliwa.
Powered by Blogger.